Friday, August 28, 2020

SARAFU ZA MIAKA 1,100 ZAGUNDULIWA HUKO ISRAEL


 Vijana waliojitolea kuchimba katika hazina ya kiakiolojia Israel wamebaini sarafu 425 ambazo zilikuwa zimezikwa kwenye chungu cha udongo kwa miaka 1,100.

Pesa nyingi zilizopatikana ni za wakati wa kipindi cha awali cha Uislamu, sehemu hiyo ilipokuwa chini ya Khalifa Abbasid.

Sarafu hizo zenye uzito wa gramu 845 bila shaka wakati zinazikwa zilikuwa na thamani kubwa - kiasi cha kununua jumba la kifahari katika moja ya miji ya Khalifa.

Je ni nani aliyekuwa anamiliki sarafu hizo na kwanini hakurejea kuchukua tena pesa hizo, ni baadhi ya maswali ambayo bado ni fumbo.

"Mtu aliyezika hazina hii miaka 1,100 bila shaka alitarajia kwamba atarejea kuzichukua, na hata kuchukua chungu na msumari wake ili kisiweze kusogea," wakurugenzi wa machimbo, Liat Nadav-Ziv na Elie Haddad kutoka Mamlaka ya vitu vya kale vya Israel, wamesema hivyo kwenye taarifa iliyotolewa.

Waliongeza: "Kupata sarafu za dhahabu, kwa kiwango hicho, ni jambo nadra sana. Ni fedha ambazo huwa hazipatikani katika hifadhi ya vitu vya kale, hasa ukizingatia kwamba dhahabu imekuwa kitu cha thamani sana, pesa zilizoyeyushwa na kutumiwa tena kutoka kizazi kimoja hadi kingine."

Vijana waliovumbua sarafu hizo, Oz Cohen, amesema: "Lilikuwa jambo la kufurahisha. Nilichimba chini ya ardhi na nilipochimbua, niliona kile kilichoonekana kama majani. Nilipoangalia tena nikaona ni sarafu za dhahabu."

Robert Kool, mtaalamu wa sarafu, amesema kuwa sarafu hizo zilijumuisha dinari za dhahabu lakini pia vipande vidogo vya dahabu 270 - vipande vya dinari vilitumika kama "salio la kiwango cha chini".

Aliongeza kwamba moja ya vipande ilikuwa ni dhahabu iitwayo solidus za wakati wa Byzantine wa mfalme Theophilos zilizotengenezwa Constantinople, ambazo zilikuwa nyenzo adimu sana kuendeleza uhusiano kati ya milki mbili hasimu wakati wa kipindi hicho. (Chanzo BBC Swahili)

No comments: